Ndugu waandishi wa habari;
LEO tumewaita hapa ili kuwaomba mtufikishie ujumbe kwa Watanzania, kwamba nikiwa mwanasheria na mtu ambaye nimepata ujuzi wa kazi za ushushu, nimefanya uchunguzi matukio haya ya utekaji na utesaji na kugundua mambo mengi mno.
Uchunguzi huu nimeufanya kabla na baada ya kukamatwa kwa Mkurugenzi wetu wa Ulinzi na Usalama, Willifred Muganyizi Lwakatare, ambaye hivi sasa anashitakiwa mahakamani kwa tuhuma za kupanga ugaidi.
Nimefanya hivyo kwa kuangalia maslahi mapana ya taifa langu na chama changu. Katika uchunguzi wangu huo, nimegundua mambo mengi ikiwamo kuwapo kwa genge la watu ndani ya serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM), wanaopanga mipango hii ya kishetani na kisha kuwasingizia watu wengine.