ADV

ADV

ADVERTISEMENT CORNER

HUDUMA YA KUKATA TICKET ZA NDEGE ONLINE


SOMA HABARI

SOMA HABARI

Saturday, December 22, 2012

Azua Taharuki Kwa Kupanda Nguzo Ya Umeme




MTU mmoja aliyetambuliwa kwa jina la Shija Machiya (30), mkazi wa Kijiji cha Butulwa, Kata ya Old Shinyanga jana alizua kizaazaa, baada ya kupanda kwenye nguzo ya umeme ya njia kuu inayopeleka umeme mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu wilayani Kahama.
Machiya alipanda katika nguzo hiyo inayosafirisha umeme wa msongo wa KV 220 katika eneo la Ihapa jirani na Kiwanda cha Nyama na kusababisha taharuki kwa wakazi wa maeneo hayo.
Tukio hilo lilitokea saa5 asubuhi, ambapo wakazi wa eneo hilo waliacha shughuli zao kwa muda wakifuatilia tukio hilo pamoja na kuhofia maisha mtu huyo.
Mama mzazi wa Machiya, Mondesta Madirisha, alisema kuwa kwa kipindi cha wiki moja mtoto wake huyo alikuwa akisumbuliwa na tatizo la kuchanganyikiwa akili.
Alisema kuwa wanahisi kuwa tatizo hilo lilitokana na kuugua malaria ambapo waliamua kumpatia dawa za kienyeji na hali yake ilionyesha kuwa ni ya kuridhisha.
“Tulipompa dawa ya kienyeji alipona kabisa, lakini jana tu kwenye mida ya saa mbili asubuhi, hali yake ilibadilika ghafla. Alianza kupiga kelele, akatoroka nyumbani na kuanza kukimbia ovyo barabarani, hali ambayo ilisababisha baadhi ya wananchi kuanza kumfuata,”alisema Madirisha na kuongeza:
“Mimi nilikuwa nikitokea shamba, ghafla nilikutana naye akikimbia mbio. Nilimsemesha na kumwomba asimame, lakini alikataa na kukimbilia kulipokuwa na watu wakilima. Niliwaomba msaada wamkamate, lakini aliwazidi mbio na hapo hapo aliamua kupanda katika nguzo ya umeme na kwenda juu kabisa, ndiyo huko mlipomuona.”
Alifafanua kuwa baada ya kuona hali hiyo waliamua kutoa taarifa kwa viongozi wa Serikali ya kitongoji na kijiji, ambao waliliarifu Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), waliofika katika eneo la tukio, kisha kuwasiliana na Polisi pamoja watu kikosi cha zimamoto.
Juhudi za kumshusha kijana huyo kwenye nguzo hiyo zilifanyika huku Machiya akirajibu kukwepa kwa kupanda juu zaidi ya nguzo, ambapo pia aliamua kuvua nguo zake zote.
Hata hivyo Tanesco kushirikiana na Zimamoto walifanikiwa kumshusha kijana huyo bila madhara yoyote.
Akizungumzia tukio hilo, Mhandisi wa Njia Kuu za Umeme mkoani Shinyanga, Job Bidya alisema kuwa kitendo hicho cha Machiya kupanda katika nguzo za umeme kingeweza kuhatarisha uhai wake kutokana na njia hiyo kupitisha umeme mkubwa wa msongo wa KV. 220.
Alisema kuwa baada ya kupata taarifa za tukio hilo, walilazimika kuzima umeme na kufika eneo hilo kisha juhudi za kumteremsha kijana huyo zilifanyika kwa ushirikiano wa kikosi cha zimamoto na uokoaji Manispaa ya Shinyanga, Jeshi la Polisi na wananchi.
Jeshi la polisi mkoani Shinyanga limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba kijana huyo anashikiliwa kwa uchunguzi zaidi ili kujua iwapo alifanya kitendo hicho kwa kuchanganyikiwa au kwa makusudi.
 MWANANCHI

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...