Taratibu za matibabu
ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho
Kikwete, zimekamilika Jana, Jumatatu, Novemba 24, 2014.
Taratibu hizo za
matibabu za Mheshimiwa Rais Kikwete zimekamilika kiasi cha saa 12
asubuhi ya leo wakati madaktari bingwa katika Hospitali ya Johns Hopkins
iliyoko mjini Baltimore, Jimbo la Maryland, Marekani, walipomfanyia
hatua ya mwisho ya tiba.
Hata hivyo, Rais
Kikwete ataendelea kupumzika na kuangaliwa kwenye Hoteli Maalum
inayohusiana na Hospitali ya Johns Hopkins kwa siku mbili hadi tatu
kabla ya kuanza safari ya kurejea nyumbani.
Kama kila kitu kitakwenda kama ilivyopangwa na madaktari, Rais Kikwete anatarajiwa kurejea nyumbani Jumamosi, Novemba 29, 2014.
Rais Kikwete
aliondoka nchini Alhamisi ya Novemba 6, 2014, kwenda kufanyiwa uchunguzi
wa afya yake lakini madaktari katika Hospitali ya Johns Hopkins
waliamua kumfanyia upasuaji wa tezi dume Jumamosi ya Novemba 8, 2014.
Rais Kikwete
anaendelea kuwashukuru Watanzania kwa sala na maombi yao ya kumtakia
heri ya kupona haraka na kurejesha afya njema katika kipindi chote cha
ugonjwa wake.
No comments:
Post a Comment