ADV

ADV

ADVERTISEMENT CORNER

HUDUMA YA KUKATA TICKET ZA NDEGE ONLINE


SOMA HABARI

SOMA HABARI

Friday, February 13, 2015

Mtihani mgumu Ukawa


Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju amesema madai ya wadau ya kutaka Tume Huru ya Uchaguzi, mgombea binafsi na haki ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa urais mahakamani, yatafanyiwa kazi iwapo Katiba Inayopendekezwa itapitishwa kwenye Kura ya Maoni Aprili 30.
Jambo hilo ni mtihani mgumu kwa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) ambao umetangaza kususia kuipigia kura Katiba Inayopendekezwa huku ikitaka mambo hayo matatu yafanyiwe kazi kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
Katika mazungumzo yake na wahariri na viongozi wa magazeti yanayochapishwa na kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) ya Mwananchi, Mwanaspoti na The Citizen jana, Masaju pia alitumia takribani saa mbili kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu suala la kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi.
Akizungumza kwenye ofisi za makao makuu ya Mwananchi Communications Tabata Relini jijini Dar es Salaam jana, Masaju alisema mambo hayo ni muhimu sana katika kipindi hiki na hivyo ni muhimu kwa wananchi kupitisha Katiba Inayopendekezwa ili masuala hayo yaandaliwe utaratibu wa kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu ujao.
Katika mkutano wa pamoja na Rais uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana, vyama vya upinzani, vikiongozwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vilitoa hoja ya kutaka mchakato wa Katiba Mpya uahirishwe hadi baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba na kwamba katika kipindi hiki Katiba ya sasa ifanyiwe marekebisho ili Tume ya Uchaguzi iwe huru, kuingiza mgombea binafsi na haki ya kupinga mahakamani matokeo ya uchaguzi wa Rais.(P.T)
"Mambo haya matatu yametambuliwa Katiba Inayopendekezwa na tunaweza kuyawekea mfumo wa kisheria ili yatekelezwe kama Katiba Inayopendekezwa itakuwa imepitishwa. Kama itapitishwa Aprili 30 na Uchaguzi Mkuu ni Oktoba, halafu tukiiweka Katiba hii kabatini (tusiitumie), tutapata shida," alisema Masaju, ambaye aliisifu Katiba Inayopendekezwa kuwa ina mambo mengi mazuri.
"Ushauri wangu kwa Serikali, kama Katiba imepigiwa kura na watu wakaipitisha, basi tuanze kutekeleza yale yanayowezekana."
Akizungumzia kipindi cha mpito cha miaka minne ambacho kimewekwa kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa Katiba hiyo alisema si lazima Katiba Inayopendekezwa ianze kutumika baada ya kipindi hicho.
"Huo ni muda tu umewekwa na si lazima ufike. Kuna mambo ya msingi ya kuzingatia. Mfano, Katiba hii imezungumzia masuala ya haki mbalimbali. Haki hizi utekelezaji wake utategemea na bajeti iliyopo. Jambo hili linahitaji muda kidogo. Kuna mambo ambayo hatuwezi kuyafanya kwa sasa, mfano ni hili la haki ya wananchi kupata maji au kuwa na zahanati kwa kuwa linahitaji bajeti kuliandaa," alisema.
Alisema yale ambayo yanahitaji bajeti kidogo au kutohitaji kabisa, kama suala la kuwapo kwa Tume Huru ya Uchaguzi, yanaweza kuanza kutekelezwa.
"Katiba ikipita kuna mambo tunayoweza kuyafanya hasa yale yanayohusu uchaguzi. Ni mambo ya msingi sana ambayo kama mkiyaacha watu watawashangaa," alisema.
"Kama watu walitaka mgombea binafsi na leo unakwenda kufanya uchaguzi na Katiba imepitishwa (inatambua mgombea binafsi), halafu huitumii, wengi watakushangaa."


No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...