ADV

ADV

ADVERTISEMENT CORNER

HUDUMA YA KUKATA TICKET ZA NDEGE ONLINE


SOMA HABARI

SOMA HABARI

Wednesday, April 10, 2013

HOTUBA YA WAZIRI MKUU, MHESHIMIWA MIZENGO PETER PINDA (MB), KUHUSU MAPITIO NA MWELEKEO WA KAZI ZA SERIKALI NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA FEDHA YA OFISI YA WAZIRI MKUU NA OFISI YA BUNGE KWA MWAKA 2013/2014


 

UTANGULIZI

1. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa Hoja kwamba kutokana na Taarifa zilizowasilishwa leo na Wenyeviti wa Kamati za Katiba, Sheria na Utawala; Kamati ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; na Kamati ya Uchumi, Viwanda na Biashara na Kamati ya Masuala ya UKIMWI na Dawa za Kulevya ndani ya Bunge lako Tukufu ambazo zimechambua Bajeti ya Mafungu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge lako sasa lipokee na kujadili Taarifa ya Mapitio ya Utekelezaji wa Kazi za Serikali kwa mwaka 2012/2013 na Mwelekeo kwa mwaka 2013/2014. Vilevile, naliomba Bunge lako Tukufu likubali kupitisha Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Taasisi zilizo chini yake pamoja na Ofisi ya Bunge kwa mwaka 2013/2014.

2. Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya kwa maslahi ya Nchi yetu. Mheshimiwa Rais ameiletea Tanzania sifa, heshima na kuiwezesha kutambulika zaidi Kimataifa katika Nyanja mbalimbali. Ziara ya kihistoria ya Mheshimiwa Xi Jinping, Rais wa Jamhuri ya Watu wa China aliyoifanya Nchini tarehe 24 hadi 25 Machi 2013 ni ushahidi tosha wa kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais ya kukuza ushirikiano wenye maslahi ya kiuchumi kati ya Nchi yetu na Nchi nyingine. Katika ziara hiyo, Mikataba 16 ya ushirikiano katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ilitiwa saini. Utekelezaji wa Miradi hiyo utachochea uwekezaji na hivyo kuongeza kasi ya ukuaji uchumi na kupunguza umaskini.

3. Mheshimiwa Spika, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge waliochaguliwa kuwa Wenyeviti na Makamu Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Bunge. Vilevile, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge waliochaguliwa kuiwakilisha Tanzania katika Taasisi mbalimbali za Kitaifa na Kimataifa. Ni matumaini yangu kwamba wote walioteuliwa na kuchaguliwa watatumia nafasi hizo kwa manufaa ya Bunge na kwa maendeleo ya Watanzania kwa ujumla. Hongereni Sana!

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...