
UTANGULIZI
1. Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa Hoja kwamba kutokana na Taarifa
zilizowasilishwa leo na Wenyeviti wa Kamati za Katiba, Sheria na Utawala; Kamati
ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa; na Kamati ya Uchumi, Viwanda na
Biashara na Kamati ya Masuala ya UKIMWI na Dawa za Kulevya ndani ya Bunge lako
Tukufu ambazo zimechambua Bajeti ya Mafungu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge lako
sasa lipokee na kujadili Taarifa ya Mapitio ya Utekelezaji wa Kazi za Serikali
kwa mwaka 2012/2013 na Mwelekeo kwa mwaka 2013/2014. Vilevile, naliomba Bunge
lako Tukufu likubali kupitisha Makadirio ya Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Waziri
Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Taasisi
zilizo chini yake pamoja na Ofisi ya Bunge kwa mwaka
2013/2014.
2. Mheshimiwa
Spika, awali ya yote napenda kumpongeza Mheshimiwa
Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi
kubwa anayoifanya kwa maslahi ya Nchi yetu. Mheshimiwa Rais ameiletea Tanzania
sifa, heshima na kuiwezesha kutambulika zaidi Kimataifa katika Nyanja
mbalimbali. Ziara ya kihistoria ya Mheshimiwa Xi Jinping, Rais wa Jamhuri ya
Watu wa China aliyoifanya Nchini tarehe 24 hadi 25 Machi 2013 ni ushahidi tosha
wa kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais ya kukuza ushirikiano wenye maslahi ya kiuchumi
kati ya Nchi yetu na Nchi nyingine. Katika ziara hiyo, Mikataba 16 ya
ushirikiano katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo ilitiwa saini. Utekelezaji
wa Miradi hiyo utachochea uwekezaji na hivyo kuongeza kasi ya ukuaji uchumi na
kupunguza umaskini.
3. Mheshimiwa
Spika, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge
waliochaguliwa kuwa Wenyeviti na Makamu Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Bunge.
Vilevile, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge waliochaguliwa kuiwakilisha Tanzania
katika Taasisi mbalimbali za Kitaifa na Kimataifa. Ni matumaini yangu kwamba
wote walioteuliwa na kuchaguliwa watatumia nafasi hizo kwa manufaa ya Bunge na
kwa maendeleo ya Watanzania kwa ujumla. Hongereni
Sana!
No comments:
Post a Comment