Na Boniface Meena na Sharon Sauwa, Mwananchi
Dodoma. Kwa mara ya pili, Spika
Anne Makinda jana alilazimika kuahirisha kwa muda shughuli za Bunge la
Jamhuri ya Muungano baada ya wabunge wa vyama vya upinzani kukataa
kukaa, wakishinikiza kitendo cha polisi kumpiga na baadaye kumkamata
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kijadiliwe kwa masilahi ya
Taifa.
Profesa Lipumba, ambaye pamoja na wanachama
wengine 32 walikamatwa juzi eneo la Mtoni Mtongani wakati alipokuwa
akielekea Zakhem, Mbagala jijini Dar es Salaam kuwataka wafuasi wa CUF
kutawanyika kwa amani baada ya Jeshi la Polisi kuzuia maandamano, jana
alikamatwa tena akiwa nje ya Kituo Kikuu cha Polisi muda mfupi baada ya
kuachiwa kwa dhamana, akidaiwa kuongea na waandishi wa habari wakati
akiwa mtuhumiwa.
Wakati akiwa mbaroni, Profesa Lipumba alijisikia
vibaya na hivyo kupelekwa hospitali kabla ya kufikishwa Mahakama ya
Kisutu jioni, akishtakiwa kwa kufanya maandamano bila ya kibali.
Jana bungeni, Spika Makinda alijikuta akipambana
na nguvu ya wabunge wachache wa upinzani ya kuzuia kuendelea kwa
shughuli za Bunge kama ilivyokuwa mwishoni mwa mwaka jana wakati
walipotumia staili hiyo ya kusimama wakati wote kushinikiza Bunge
kusikiliza matakwa yao kuhusu hatua za kuchukua dhidi ya wahusika kwenye
sakata la uchotwaji fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow.
Wakati huo ilibidi Waziri Mkuu Mizengo Pinda na
Waziri wa Nchi, Sera na Utaratibu wa Bunge, William Lukuvi kumfuata mkuu
wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe kuzungumza naye kabla ya
Bunge kuahirishwa.
Tafrani ya jana iliyodumu kwa dakika 12 na sekunde
8 ilianza baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu. Baada
ya kumalizika kwa kipindi hicho, wabunge zaidi ya watano wa upinzani
walisimama kutaka kutoa hoja na Spika Makinda alimpa nafasi ya kwanza
James Mbatia, ambaye ni mbunge wa kuteuliwa, aliyeomba mwongozo akitumia
Kanuni ya 47 inayohusu kuahirishwa kwa shughuli za Bunge ili kujadili
jambo la dharura.
Mbatia, ambaye aliisoma kanuni yote ya 47 yenye
vipengele vinne, aliomba kutoa hoja ya kutaka kitendo cha kupigwa kwa
Profesa Lipumba wakati akiwa katika mkutano wa hadhara, kijadiliwe.
Mbatia alisema: “Jana (juzi) tarehe 27 mwezi
Januari mwaka huu wilayani Temeke jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa
CUF Profesa Lipumba alikuwa na ratiba ya kufanya mkutano wa hadhara
pamoja na maandamano na walifuata taratibu zote za kisheria na za
kikatiba za kujumuika, kuandamana na kuweza kubadilishana mawazo.
“Cha kushangaza, dakika za mwisho polisi
walikataza jambo hilo lisiendelee na Profesa Lipumba akaonyesha
ushirikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kutoendelea na jambo hilo, lakini
Jeshi la Polisi likafika baadaye kidogo kuamua kutumia nguvu dhidi ya
raia ambao hawafanyi fujo yoyote, raia ambao wameonyesha ushirikiano na
utii kwa Jeshi la Polisi.”
Mbatia alisema pamoja na ushirikiano huo polisi
waliamua kumpiga Profesa Lipumba na raia wengine wa Tanzania hata watoto
wadogo chini ya umri wa miaka mitano, kauli ambayo ilifanya wabunge
wampigie makofi mwenyekiti huyo wa Chama cha NCCR-Mageuzi.
Aliendelea kusema waandishi wa habari walipigwa virungu na kudhalilishwa, jambo ambalo alisema linaondoa utulivu, amani nchini.
“Mimi binafsi nilisikitika sana baada ya vyombo
vya habari kuonyesha moja kwa moja. Nilichukua hatua ya kuwasiliana na
Waziri wa Mambo ya Ndani kwa kuwa mambo ya aina hii yalipokuwa yakitokea
huko nyuma, sisi vyama vya siasa tuliwahi kumuhusisha hata Rais.”
No comments:
Post a Comment