Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Posted Alhamisi,Marchi12 2015 saa 9:58 AM
Posted Alhamisi,Marchi12 2015 saa 9:58 AM
Kwa ufupi
Mwenyewe asisitiza kwamba hana taarifa rasmi, ataendelea kufanyakazi kama kawaida
Dar/Kigoma. Siku moja baada ya Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kutangaza kumvua uanachama, Mbunge wa
Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kesho atatua jimboni kwake kuzungumza na
wananchi kupitia mikutano ya hadhara.
Uamuzi wa kumfukuza Zitto (pichani) ulifikiwa juzi
ikiwa ni muda mfupi baada ya Mahakama Kuu kutupilia mbali kesi
aliyofungua Januari 2, 2014, dhidi ya Bodi ya Wadhamini na katibu mkuu
wa Chadema, iliyokuwa imeshikilia uanachama wake.
Mwanasheria mkuu wa Chadema, Tundu Lissu ndiye
alitangaza kutimuliwa kwa Zitto akisema ni kutokana na kufungua kesi
mahakamani, kinyume na Katiba ya Chadema kipengele cha 8 (a) (x).
Jana, Zitto ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya
Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) aliongoza kikao cha kamati hiyo,
kilichojadili taarifa ya Tanesco na baadaye alisisitiza kwamba hana
taarifa rasmi ya uamuzi wa mahakama na atakapoipata atazungumzia hatima
yake.
“Kama mnavyoona mimi naendelea na kazi na wala
sina taarifa rasmi lakini nikipata taarifa rasmi na mimi nitatoa taarifa
rasmi, Ijumaa (kesho) ninakwenda jimboni kuzungumza na wapigakura wangu
ambao niliwaahidi kufanya hivyo kabla ya vikao vya Bunge kuanza Jumanne
ijayo,” alisema Zitto ambaye taarifa zinasema alikuwa amepapanga
kuwaaga wapiga kura na baadaye kutimkia kwenye chama kipya cha ACT
alichokiasisi.
“Muhimu kwangu ni kufanya kazi ya Watanzania na
nitafanya kwa mazingira yoyote yale. Siasa yangu inajikita katika
masuala, siyo watu, ukiandika kuhusu Zitto siyo kwa ajili ya mtu bali
masilahi ya Taifa.
“Nakuzwa, nakomazwa na hii ni changamoto, nitaendelea kufanya kazi zangu hadi nitakapopata taarifa rasmi.”
Mwanasheria wa Zitto, Albert Msando juzi
aliliambia gazeti hili kwamba, anafuatilia uamuzi huo wa mahakama kabla
ya kuona ni hatua gani watazichukua.
ACT wachekelea
Baadhi ya wanachama na viongozi wa Chama cha ACT
mkoani Kigoma wamedai kufurahishwa na uamuzi huo, wakidai kuwa
utakinufaisha chama hicho.
Mkazi wa Mwandiga, Dunia Pemba alisema Zitto
alipaswa kujiondoa ndani ya Chadema pale tu alipovuliwa nyadhifa zake
ili atazame sehemu nyingine yenye demokrasia pana kwa vile chama hicho
kilionyesha hakimhitaji tena.
“Sisi tulitangulia huku ACT na sasa tunamsubiri
kwa hamu, aje kujenga chama hiki ambacho ni tishio kubwa hapa nchini na
bila shaka kitachukua viti vingi vya ubunge katika Uchaguzi Mkuu wa
mwaka huu, ndiyo maana kutimuliwa kwa Zitto Kabwe ni faraja kwetu kwa
sababu atapata muda wa kutosha kujenga chama,” alisema Pemba.
Source: Mwananchi
Source: Mwananchi
No comments:
Post a Comment